Sunday, March 24, 2019

ENEO LA MAPENZI : Ulipo sasa, Unakotaka Kufika, Viwango vya Kujiwekea . Kitabu cha Kusoma.

Hili ni eneo linalohusu mahusiano yako ya kimapenzi na mwenza wako. Ni eneo muhimu sana kwa sababu hili linagusa kila eneo la maisha yetu. Kama mahusiano yako ya kimapenzi yako vizuri basi maisha yako yanakuwa vizuri. Lakini kama eneo hili lina matatizo, hutaweza kutuliza akili yako kwenye jambo lolote.

ULIPO SASA; Tafakari pale ulipo sasa kwenye mahusiano yako ya kimapenzi, je umeoa au kuolewa au upo peke yako? Na je kwenye hali ya mahusiano uliyopo, unayafurahia? Unayaelezeaje mapenzi? Ni kitu gani unatoa na kipi unapokea kutoka kwenye mahusiano yako ya mapenzi? Je unaamini mapenzi yanaleta maumivu? Je upo tayari kumpenda kweli mwenzako na kumwonesha kwamba unampenda? Je unajiona ni mtu unayestahili kupendwa kweli? Jiulize na kujipa majibu ya maswali hayo na yatakupa picha ya pale ulipo sasa.

UNAKOTAKA KUFIKA; Katika kuboresha zaidi mahusiano yako ya kimapenzi, unapaswa kuwa na picha ya wapi unataka mahusiano hayo yafike. Katika kutengeneza picha ya unakotaka kufika, jiulize na kujipa majibu ya maswali haya; je mahusiano bora ya kimapenzi kwako unataka yaweje? Pata picha ya mahusiano yenye mafanikio, mnawasilianaje, kuchukulianaje, vitu gani mnafanya pamoja na jinsi mnavyoyafurahia maisha pamoja. Kuwa na picha hii kila wakati na ifanyie kazi, itakusukuma kuwa bora zaidi.

VIWANGO VYA KUJIWEKA; Katika eneo la mapenzi unapaswa kujiwekea viwango ambavyo utavizingatia ili kuimarisha eneo hili. Viwango vya kujiwekea ni muda wa kuwa pamoja wewe na mwenza wako, inaweza kuwa kwenye mtoko mnaofanya pamoja, kufanya mazoezi pamoja na hata kuwa na ratiba ya kuwa na faragha nyinyi wawili pekee kwa ajili ya yale muhimu kwenu. Zingatia sana hili la kupata muda wa kuwa na mwenzako na weka kiwango cha muda huo.

KITABU CHA KUSOMA; Kujiweka vizuri kwenye eneo la mahusiano ya mapenzi soma kitabu kinachoitwa MEN ARE FROM MARS, WOMEN ARE FROM VENUS Kilichoandikwa Na John Gray. Kitabu hiki kitakufundisha jinsi ya kuishi na mwenzako.

No comments:

Post a Comment