MTAWANYIKO WA NGUVU KAZI KAMA MSINGI WA KUANZISHA BIASHARA
MOJA ya vielelezo vya
kawaida vya biashara ndogondogo mitaani ni hali ya kulazimisha kufanya
shughuli fulani na kutazamia kuwa itafanikisha jitihada za kuingiza
kipato. Kwa maana hiyo, si kila biashara ambayo inaonekana barabarani
inaweza kuitwa kuwa ingefaa kuwa hapo au kuwepo kabisa, lakini utitiri
huo wa biashara ni msingi mmojawapo muhimu wa jinsi biasbara zinavyoanza
na kukua. Mara nyingi kuna chembe ya kubahatisha, ingawa yapo maeneo
ambako ni wazi hapakuwa na wazo thabiti la biashara kuanzia mwanzo,
hivyo haisimami kabisa.
Hali hiyo ni mojawapo
kati ya vielelezo vya tofauti ya mtu anayefanya biashara na anayejaribu
kukwepa ajira, labda kwa sababu itakuwa ya sulubu au imeshindikana
kupata ajira kama hiyo. Moja ya vianzio vya ajira ni kuaminiana, hivyo
mtu asiye na mdhamini wa aina moja au nyingine pale anapotafuta
kukubalika katika aina moja au nyingine ya shughuli, inabidi 'ajiajiri
mwenyewe' kwa kuanzisha shughuli yake. Ndiyo hapo linakuja tatizo, kama
mtu hiyo ana moyo wa biashara au ni wa kutumwa, na ikiwa katika biashara
hiyo atakuwa na moyo wa kutumwa, itakwama.
`Ipo tofauti kati ya
moyo wa biashara na moyo wa kutumwa, kuwa katika biashara mtumishi wa
kwanza ni yule mwenye biashara, kuwa anatakiwa ajali kila kitu na
kuangalia kila kitu kiwe salama, wakati moyo wa kutumwa ni kinyume
chake. Mtu anayetumwa hufanya yale yanayomgusa, anayowajibika nayo au
kuulizwa, na hayo mengine yahamhusu, yakae vyema au vinginevyo suala
hilo halimhusu. Hisia ya namna hiyo inafikia tamati ya kutokuwa na moyo
wowote kuhusu shughuli nzima inayoendelea, nje ya kisehemu kidogo
ambacho mtu anakabidhiwa, ndicho anajali.
Kwa maana hiyo mtu
ambaye amezoea kuajiriwa na ana hulka ya mwajiriwa katika eneo la kazi,
hajishughulishi na chochote kile ambacho hakimgusi moja kwa moja, hawezi
kuanzisha biashara ikasimama. Mtu kama huyo anazoea lawama badala ya
kuchangia, anakwepa majukumu badala ya kusaidia kuboresha, na si ajabu
hata akawa na furaha pale mtu mwingine akikosea jambo fulani, kwani kwa
hali hiyo aonekane bora zaidi kuliko huyo mwingine. Akiinua biashara,
atabadili roho yake?
Hulka ambazo mtu anakuwa nazo kwa vipindi virefu
vya maisha baada ya kuingia ujana na hasa kuanza kupata fedha haziwezi
kubadilika ghafla kutokana na 'mahitaji' kubadilika. Hivyo uzoefu au
historia ya biashara ni kupanda na kushuka au kuanguka kwa biashara hasa
kutokana na hulka za watu wanaozianzisha, pale hisia zao na mwenendo
wao unapokuwa kikwazo katika biashara yenyewe. Ni tatizo ambalo kwa
kiasi fulani lipo hata katika biashara zilizofaulu, kuwa kuna wakati
anatokea mtu aajiriwe kama meneja halafu mambo yaende vizuri, baadaye
aje mwingine, iporomoke. Katika biashara ndogo, ni biashara yenyewe
inayokufa.
Ndiyo maana idadi kubwa
ya biashara zinaandikishwa na hata kuanza, lakini nyingi zinadidimia
baada ya muda si mrefu, kwani walioanzisha hawalingani kisaikolojia na
shughuli wanayoianzisha. Ni hali inayoonekana katika nyanja zote za
jamii, na mara nyingine utasikia mtu akieleza jinsi alivyohangaika hadi
kipindi fulani akaanza biashara inayoendana na hisia zake, inayomfaa, au
kupata kazi ambayo anaendana nayo. Akiondolewa katika nafasi hiyo, hasa
kama bado ni kijana anayeangalia zaidi haiba yake (nafasi yake
kijamii), anaweza kuporomoka.
Ndiyo maana ukiona
biashara imesimama mahali fulani, usikimbilie kudhania kuwa mradi
imesheheni basi imefaulu, ila kutambua kuwa kuna 'moyo unadunda,' au kwa
lugha ya kitaaluma ni 'half life,' kuwa kitu kinachipuka, kichanue
halafu kififie, labda kama kitaota mizizi, kiwe endelevu. Ukitafakari ni
biashara ngapi unazoona ambazo zimechanua tu na hazina mizizi, na
badala ya kuwa endelevu huenda ziko mbioni kunyauka, utashangaa, na siyo
rahisi kusema kuwa huyu alikosea hiki au kile. Masuala mengine ni ya
kimazingira, kwa mfano ni wapi mtu aweke biashara yake, achuuze bidhaa
gani au atengeneze nini, kila kitu hutegemea kingine; biashara inakuwa
ni kama wazo linachipuka, liinuke au ligonge mwamba.
CHANZO CHA HABARI:GAZETI LA MAJIRA,NA JOHN KIMBUTE, Jumatatu , Januari 20 , 2014.
No comments:
Post a Comment