Monday, December 30, 2019

USITOE USHAURI KWA MTU AMBAYE HAJAKUOMBA , USICHUKUE USHAURI KWA AMBAYE HUJAMWOMBA.

Ushauri ni kitu ambacho unapaswa kuwa nacho makini sana wakati wa kutoa na hata kutokea.

Tuanze na kutoa, kamwe usitoe ushauri kwa mtu ambaye hajakuomba umshauri, unaweza kuona unamsaidia mtu huyo, lakini utakuwa unapoteza muda wako bure. Watu huwa hawafanyii kazi ushauri ambao hawajautafuta wenyewe. Unaweza kumwona mtu yupo kwenye hali fulani na kufikiri ushauri wako utamsaidia, ukamshauri vizuri na ukashangaa hafanyii kazi yale uliyomshauri. Hii ni kwa sababu mtu huyo hajawa na maumivu ya kutosha kumsukuma kutaka kutoka pale alipo sasa na ushauri wako ni kelele tu kwake. Mtu anayekuja kwako na kukuomba ushauri, ni mtu ambaye ameshaumia vya kutosha na anataka njia ya kuondoka kwenye maumivu, huyu ukimshauri anazingatia. Hivyo kama mtu hajakuomba ushauri, usijisumbue kutoa ushauri wako.

Tukienda kwenye kupokea ushauri, usichukue ushauri wa mtu ambaye hujamwomba akushauri. Hii ni kwa sababu mtu anaweza kuona jambo fulani kwa nje na akajumuisha kwamba tatizo lako ni hili na hatua za kuchukua ni hizi. Lakini mtu huyo anakuwa hajajua kwa undani unapitia nini hivyo ushauri huo unakuwa siyo sahihi. Kama unataka ushauri, mtafute mtu ambaye unamwamini, mweleze kile unachopitia bila ya kuficha chochote, kisha yeye awe na taarifa sahihi na kukushauri kwa usahihi. Lakini siyo ule ushauri wa juu juu ambao watu wanatoa kwa kuona mambo ya nje bila kujua yale ya ndani.
Huwa nasema ushauri wa bure utaona gharama yake pale unapoanza kuufanyia kazi. Huwa siyo ushauri sahihi. Hivyo chukua ushauri kwa watu ambao ni sahihi, watu wenye uzoefu au ujuzi na ambao wanaielewa hali yako. Na siyo kuchukua ushauri kwa kila anayekuambia ungefanya hivi au ungefanya vile. Kadhalika usikimbilie kutoa ushauri kwa mtu ambaye hajakuomba, kwa sababu unakuwa hujaelewa kwa undani anapitia nini na utakachomshauri hatofanyia kazi.
Wapo wanaosema mbona mimi natoa ushauri kupitia makala hizi wakati sijaombwa. Ukweli ni kwamba mimi sijakuletea maarifa haya nyumbani kwako, au kukulazimisha usome, bali wewe umeyatafuta au kukutana nayo na kuona yanakufaa, hivyo ukasoma. Kuna wengi wanakutana na maarifa haya, lakini wanayapita, kwa sababu hayana maana au umuhimu kwao. Lakini wewe umeyapokea, kwa sababu kuna kitu unatafuta na hivyo unayathamini. Hivyo wajibu wangu ni kushirikisha maarifa sahihi ambayo mtu akiyatumia anaweza kupiga hatua kwenye maisha yake, lakini siwezi kumlazimisha mtu asome au kuchukua hatua.

No comments:

Post a Comment