Monday, December 30, 2019

USIJISUMBUE KUWABADILISHA WATU , WATU HUWA HAWABADILISHWI

Watu huwa hawapendi kubadilishwa, na wakigundua mtu anataka kuwabadilisha basi wanaleta upinzani mkubwa kuhakikisha hilo halitokei.
Watu huwa wanaweza kubadilika kama watachagua kubadilika wao wenyewe, lakini siyo kulazimishwa kubadilika, hivyo ndivyo saikolojia ya binadamu ilivyo.
Hivyo usijisumbue kumbadili mtu yeyote yule, hutaweza, utaishia kuibua tu migogoro isiyo na manufaa.
Kama unataka mtu mwenye sifa fulani, mtafute mtu mwenye sifa hizo na siyo kumchukua yeyote na kujiambia utambadilisha, unajidanganya.
Kwenye mahusiano, iwe ni ya mapenzi au ndoa, chagua mtu ambaye sifa alizonazo sasa unaweza kwenda nazo na siyo kujiambia utambadilisha.
Kwenye ushirikiano wa biashara au kazi, chagua kushirikiana na mtu ambaye sifa unazoziona sasa kwake unaweza kwenda nazo.
Na hata unapoajiri, angalia sifa ambazo mtu anazo na kama unaweza kwenda nazo.
Usijidanganye kwamba sifa fulani ambayo mtu anayo unaweza kuibadili, unatafuta matatizo wewe mwenyewe.
Mtu mmoja amewahi kuulizwa anawezaje kuwafanya wafanyakazi wake kuwa na tabia nzuri, alijibu kwa kusema; “siwaambii wafanyakazi wawe na tabia nzuri, bali naajiri watu ambao tayari wana tabia nzuri”.

No comments:

Post a Comment