Monday, December 30, 2019

USIANZE SIKU YAKO KWA KUFUATILIA HABARI.

Habari nyingi ni hasi au zenye kuibua hisia kwa wafuatiliaji wake. Fungulia chombo chochote cha habari au tembelea mtandao wowote unaotoa habari na utaona habari gani zinapewa kipaumbele. Ni habari za kutisha au kusisimua. Habari za mauaji, ajali, mapigano, wizi, utekaji, ukatili na nyingine kama hizo.
Unapoianza siku yako kwa habari za aina hii, unavuruga kabisa akili yako. Unajikuta umepata hasira au kukata tamaa na kuona dunia haina maana. Hata mambo ambayo ulipanga kuyafanya hutaweza kuyafanya kwa hamasa kubwa pale ambapo umeshakutana na habari za kutisha au kukatisha tamaa.
Ndiyo maana nakushauri usianze siku yako kwa habari, sijakuambia usifuatilie kabisa habari (japo hilo ni jema ukiliweza), ila usianze nazo kwenye siku yako. Anza siku yako kwa kusali/kutahajudi, kusoma vitabu, kupangilia siku yako na kisha kuanza majukumu muhimu kwako kikazi au kibiashara. Mwisho wa siku wakati umeshakamilisha yale muhimu, hapo sasa unaweza kupitia habari ili ujue nini kinaendelea.
Ukifanya hivi utajikuta unakuwa na siku tulivu, siku ambayo umeweka umakini wako kwenye yale muhimu kwako kufanya na siyo kuvurugwa na habari za mambo yanayoendelea, ambayo hayakuhusu moja kwa moja.
Wapo wanaosema ni muhimu kuanza na habari kwa sababu kunaweza kuwa na kitu muhimu unapaswa kujua kabla siku haijaanza, labda kuna daraja limeharibika hivyo usipoanzana habari hutajua. Nasema hiyo siyo sababu yenye mashiko ya kuruhusu siku yako ichafuliwe na habari nyingi hasi. Na nikuambie kitu kimoja rafiki yangu, kama kuna habari muhimu kweli, itakufikia hata kama hufuatilii habari. Tukienda na mfano huo wa daraja kuharibika, hivi unafikiri unahitaji chombo cha habari kujua hilo? Kila mtu atakuwa anazungumzia hilo na hivyo utajua tu.
Kadhalika kwa habari nyingine ambazo ni muhimu, wale wanaokuzunguka watakuwa wanazizungumzia, hivyo kama ni kitu chenye umuhimu utakijua tu.
Usikubali kuharibu siku yako kwa kuanza na habari, anza siku yako kwa mipango yako na kisha imalize kwa habari.

No comments:

Post a Comment