Tuesday, June 1, 2021

KUJUA KUSUDI LAKO SEMA NDIYO , KUISHI KUISHI KUSUDI LAKO SEMA HAPANA.

VITU VIWILI VYA KUFANYIA KAZI KWENYE MAISHA YAKO.

Ili uweze kufikia mafanikio makubwa na kuacha alama hapa duniani, kuna vitu viwili vikubwa unavyopaswa kuvifanyia kazi. Nimeweza kuja na vitu hivi viwili baada ya kujifunza na kutafakari kwa kina na kuona jinsi watu wanahangaika na mambo mengi lakini hawapati matokeo yoyote makubwa.

Ukiamua kuachana na mengine yote unayohangaika nayo na kufanyia kazi haya mawili tu, utaacha alama kubwa hapa duniani.

Mambo hayo mawili ni KUJUA NA KUISHI KUSUDI LAKO na KUWA NA NDOTO KUBWA unazofanyia kazi kwenye maisha yako. Haya mawili tu ndiyo yanahitaji muda, umakini na nguvu zako zote ili uweze kufanya makubwa.

KUSUDI LA MAISHA YAKO.

Mark Twain amewahi kusema kuna siku mbili muhimu kwenye maisha ya mwanadamu, siku ya kuzaliwa kwake na siku anayojua kwa nini amezaliwa.

Kila mtu huwa anazaliwa, ndiyo njia pekee ya kuja hapa duniani. Lakini ni wachache sana wanaojua kwa nini walizaliwa na hao ndiyo wanaoleta matokeo makubwa na kuacha alama hapa duniani.

Ubaya ni kwamba kujua kwa nini umezaliwa ni wajibu wako mwenyewe, hakuna anayeweza kukufundisha wala kukuambia. Hata wazazi waliokuzaa hawajui kwa nini ulizaliwa. Walimu wanaokufundisha ndiyo kabisa wanaharibu, maana wanakulazimisha uwe kitu kingine na siyo wewe.

Unahitaji mabadiliko makubwa kwenye maisha yako ili uweze kujua kwa nini ulizaliwa, unahitaji kuvunja mazoea mengi uliyojenga kwenye maisha yako ili uweze kuisikiliza sauti ya ndani yako na kujua kwa nini uko hapa duniani.

Wengi hawajui kusudi la maisha yao kwa sababu wameamini kile ambacho jamii na mfumo wa elimu umewalisha kwa miaka mingi. Kama shule ilikuambia umefeli kwa sababu huna akili, unaamini hivyo kwamba huna akili. Wakati shule haiwezi kupima uwezo mkubwa ulio ndani yako, kitu ambacho shule inapima ni kukariri.





KUJUA KUSUDI, SEMA NDIYO KWA KILA KITU.

Ili uweze kujua kusudi la maisha yako unahitaji kurudi kwenye maisha ya utoto wako, na kusema ndiyo kwa kila kinachokuja mbele yako. Jaribu mambo mengi uwezavyo, fanya kila kinachokuvutia kufanya na kadiri unavyofanya hivyo utaona kuna vitu unapenda kuvifanya vizuri zaidi na watu wanavifurahia unapovifanya. Hapo ndipo utajua kusudi lako lilipo na kuweza kulifanyia kazi.






















Hivyo fanya zoezi hili rafiki yangu, kama bado hujajua kusudi la maisha yako, chagua kipindi utakachorudi kwenye utoto wako na sema ndiyo kwa kila kitu. Kila kinachokuvutia kufanya, kifanye. Tenga muda ambao utafanya majaribio mbalimbali kwenye maisha yako na kujifunza kwenye kila unachofanya.




KUISHI KUSUDI, SEMA HAPANA.

Baada ya kujua kusudi la maisha yako, sasa unahitaji kuweka umakini wako wote kwenye kuishi hilo. Hupaswi tena kuhangaika na mambo mengine nje ya kusudi hilo.

Muda na nguvu zako vina ukomo, usipoteze kuhangaika na mambo mengine. Kuna mazuri yatakayokuja kwako na yenye fursa ya kunufaika zaidi, lazima uweze kusema hapana kwa hayo mazuri ili uweze kupata yaliyo bora kupitia kuishi kusudi lako.

Ili kuishi kusudi lako, SEMA HAPANA kwa mambo mengine yote na baki kwenye kuishi kusudi lako tu.

Baada ya mimi kujua kusudi langu lipo kwenye kufundisha wengine kupitia uandishi na ukocha, nimekuwa nasema hapana kwa mengine yote isipokuwa kusudi hili.


Ukishajua kusudi lako, yapangilie maisha yako kwa namna ambayo kuishi kusudi hilo ndiyo kipaumbele kikubwa kwako na sema hapana kwa mengine yote ambayo hayahusiani na kusudi hilo.

Ni kwa njia hiyo ndiyo unaweza kuweka umakini, muda na nguvu za kutosha kwenye kusudi lako na liweze kuleta matunda mazuri kwako.

NDOTO KUBWA YA MAISHA YAKO.

Maisha yasiyokuwa na ndoto ni maisha ambayo hayana msukumo wa kuyaishi.

Kama unataka kuacha alama hapa duniani, lazima uwe na ndoto kubwa, lazima uwe na picha ambayo hakuna anayeiona na hata ukiwaambia wengine hawaamini kama inawezekana.

Ukishakuwa na picha hiyo kubwa, unapaswa kuifanyia kazi kila siku mpaka utakapoifikia. Unapaswa kuwa tayari kutoa kafara ya kila aina kwenye maisha yako ili kufika kwenye ndoto yako kubwa.

 

No comments:

Post a Comment