Tuesday, April 26, 2016

KIPAJI , JUHUDI NA KUJIFUNZA , KIPI HUTANGULIA KATIKA BIASHARA ?




YAKO  maeneo mengi katika maisha ambako lugha ya kawaida inasaidia kuelewa kiini cha mahusiano muhimu ya maeneo tofauti, bila kuwa na utaalamu wowote kuhusu jambo hilo, ila kwa kuwaangalia watu tofauti katika shughuli hizo. Uwezo wa kufanya kazi kwa ufanisi, ambao pia ni chembe ya msingi ya kufanikisha shughuli ya kibiashara, unaelezeka kwa kanuni ya aina hiyo, kuwa watu wana uwezo wa kutofautisha nini hasa kinafanya mtu apate mafanikio, au tuseme amudu shughuli fulani. Kuna chembe ya hisia katika hali hiyo, ila huwa inaashiria ukweli.

Licha ya kuwa taaluma za kisasa zinalenga zaidi kufanyika utafiti wakilishi ili kujua mahusiano kati ya maeneo tofauti ya maisha au shughuli zinazoendana katika mantiki yake, bado nafasi ya kung'amua tu kwa kutazama haiwezi kutupwa. Ikiondolewa, sehemu kubwa ya mazungumzo ya kawaida itakwama, pale ambapo takriban kila kitu kinachozungumzwa inabidi kutanguliwe na aina fulani ya utafiti au upelelezi kubakikisha kuwa ni hivyo msemaji anavyodhani, na atakayesikia hilo hawezi kujibu hadi ahakikishe utafiti wa msemaji kuwa ni sahihi. Ingekuwa taabu.

Moja ya maeneo ambako uwezo wa kung'amua mahusiano halisi yakoje ni katika kufanikisha biashara, au kumudu kitu ambacho kwa jumla ni kipya, na ambacho kinategemea uwezo wa huyo anayekishika, siyo msimamizi wala mwenye mali mwingine. Ni kwa njia gani ambako kipaji alicho nacho mtu kinatangulia, au ni juhudi zale licha ya kuwepo kipaji cha juu au cha kati, au labda ni kujifunza na kuelewa nini cha kufanya kwa muda mfupi kuliko mwingine? Je maeneo haya matatu ni tofauti kabisa au ni jambo moja ambalo linajieleza tu kwa sura tofauti?

Njia nyingine ya kufafanua suala hilo ni kulibadilisha katika mafungu, kama chembe hizo zinaenda pamoja, kwa mfano kama kila mwenye kipaji ana juhudi, au huenda hana juhudi ila afaulu kwa kipaji chake. Pia unaweza kuuliza kama kila mwenye kipaji hujifunza haraka, au labda aliye na kipaji anaelewa kwa kuangalia tu na hahitaji kujifunza, kwani 'inaandikika' kichwani akiona tu nini kinatendeka. Ni kwa njia hiyo pia unaweza kuuliza kama mwenye juhudi anajifunza haraka, au juhudi inajazia pale ambako yako mambo hayaelewi vyema ila anazingatia kanuni.
Ni wazi katika mpangilio huo wa kutoa na kujumlisha kuwa kipaji kina uwezo zaidi wa kusimama peke yake bila juhudi halisi kuwepo, ambayo haina maana kuwa mwenye kipaji hahitaji kufanya juhudi. Maana yake ni kuwa kipaji ndicho hasa nyenzo ya msingi ya kila jambo, kinachomfanya mtu awe 'anafaa' katika eneo fulani kwani silika zake na hisia zake zinaendana na jambo hilo. Ikiwa kuna upungufu wa wazi wa kipaji, suala la kujazia kwa juhudi linakuwa tatizo, na pa haiwezekani kuongeza uwezo wa kujifunza kama kipaji kimepungua sana, ila kuna uwezekano wa kuongezea uwezo wa kipaji pale elimu inapokuwa imeongezeka.

Cha kushangaza, au labda cha kujiuliza, ni jinsi gani watu wanaangaliwa katika maeneo ya kazi, na hapa inakuwa ni tatizo kama chanzo na matokeo ni kitu kile kile au ni tofauti.. Kwa mfano mtu anayesifiwa katika jambo fulani mara nyingi zaidi anasifiwa kwa kipaji chake, uwezo mahiri wa kufanya jambo, na siyo kiasi alichojifunza, au bidii anayoweka katika jambo hilo. Ila anapolaumiwa au tuseme kukosolewa katika kile anachokifanya, ni nadra kuona fikra ya anayemtazama iwe imeelekea katika kipaji chake, ila laweama zitalenga juhudi zake, uvivu, kutosikia.

Hapo ndipo linapokuja tatizo la uhusiano wa mantiki ya kawaida ya mazungumzo na hali halisi ya kitu, na kama mantiki ya kawaida inarahisisha tu kuelewana tunavyohisi kuhusu jambo fulani, kukiwa kuna upana tu wa 'makosa' katika kile tunachoona kwa kukitazama kwa macho, au tunakaribia ukweli. Unachoweza kuyanikinisha ni kuwa mantiki ya kawaida inatoa elimu maridhawa kuhusu jambo fulani, lakini siyo lazima ipatie kwa usahihi halisi wa kimantiki. Kuna viwango tofauti za 'kuachana' kwa mazungumzo na ukweli, ambavyo vinafanana na tatizo hili la kipaji, juhudi na kujifunza - kipaji cha mzungumzaji, ikiwa ni mkweli, n.k.

Suala la kipaji mara nyingi halianzii tu katika uwezo wa kuelewa cha kufanya kwa haraka ila pia kuchangamkia jambo hilo, kuwa na mwito nalo, ambao mara nyingi huendana na kipaji cha jambo hilo. Ndiyo maana biashara mara inatakiwa iwe ni kitu mtu anafanya kwa kuwa kinamfurahisha kukifanya, na siyo kwa shurti la njaa au umaskini, kwani katika hali hiyo shughuli ile itakuwa mzigo kwake. Kipaji cha kwanza ni kukipenda kitu kinachohusika ambacho kinafungua milango ya juhudi ya kujituma na kuelewa pale anapojifunza zaidi. Ni wazi asiye na juhudi halisi ana walakini wa msingi wa kutopenda anachokifanya; asiyeelewa vile vile hakipendi.

CHANZO  CHA  HABARI:  GAZETI  LA  MAJIRA  NA  JOHN  KIMBUTE ,Jumatatu, Januari ,20,2014.

No comments:

Post a Comment