Wanasema
 unaweza kulalamika huna viatu, ila ni mpaka siku utakayokutana na mtu 
asiye na miguu ndiyo utakumbuka kushukuru kwamba angalau wewe una miguu 
na hivyo viatu haviwi tatizo tena kwako.Ni
 kawaida kwetu binadamu kuzoea vitu tulivyonavyo na kuvichukulia 
kawaida, kwa sababu tumekuwa tunaviona kila siku. Lakini vitu hivyo 
hivyo tunavyovichukulia pia, kuna wengine wanavitamani kweli ila 
hawawezi kuvipata.
Moja
 ya vitu hivyo ni hizi siku tunazokuwa nazo kila siku, tangu umezaliwa 
mpaka hapo ulipofika sasa, umekua unaanza na kumaliza siku zako na hivyo
 umeshazoea, asubuhi unaamka, unaenda na shughuli zako na siku inaisha, 
unalala na kuamka tena siku inayofuata.
Kwa
 kuwa umeshazoea sana siku zako, umekuwa unajiaminisha kabisa kwamba 
kesho ipo na huchelewi kuacha kufanya kitu leo kwa kujiambia utafanya 
kesho. Ni kitu gani kinakupa uhakika kiasi hicho?
Unapopata
 habari za misiba ya watu wa karibu, wale ambao uliwajua na walikuwa na 
mipango mikubwa ila wamefariki ghafla, huwa unapata mshtuko, unaona 
kweli maisha ni mafupi. Lakini haikuchukui siku nyingi unarudi kwenye 
mazoea yako, unazichukulia siku zako poa na kuahirisha mambo.
Tunawezaje kuondokana na hali hii ili tuweze kuzipa siku zetu uzito unaostahili na kuishi kwa ukamilifu?
Mwanafalsafa
 Seneca ana mengi ya kutueleza kwenye hili. Kwenye moja ya barua 
alizoandika kwa rafiki yake Lucilius akimweleza kuhusu wengi 
wanavyokihofia kifo, aligusia hili la kuishi kila siku kwa mazoea.
Seneca
 anasema wengi wamekuwa wakijiuliza maisha yao yataenda hivyo mpaka 
lini, kila siku kulala na kuamka, kuwa na njaa na kushiba, majira ya 
masika na kiangazi. Kwa kuyatazama maisha hivyo unaona kama ni mzunguko,
 hakuna kipya, kila kitu kinajirudia.
We
 slip into this condition, while philosophy itself pushes us on, and we 
say; "How long must I endure the same things? Shall I continue to wake 
and sleep, be hungry and be cloyed, shiver and perspire?  There is an 
end to nothing; all things are connected in a sort of circle; they flee 
and they are pursued.  – Seneca 
Seneca
 anatutahadharisha kwamba tukiyaangalia maisha kwa mtazamo huo, 
tutayaona maisha ni maumivu yasiyo na mwisho, unaimaliza leo ukijua 
kesho inakwenda kuanza na kuisha kama leo. Majira ya masika yanaisha 
ukijua kiangazi kinakuja. Una njaa na kutafuta chakula kizuri kula, ila 
ukishashiba unajua kuna njaa itakuja tena. Kwa namna hii, maisha 
yanakuwa kama gereza la mateso, kusukuma siku usubiri kufa.
Lakini
 ipo namna nyingine ya kuyaangalia maisha kwa namna ambayo 
yatatunufaisha, mtazamo wa tofauti unaotusukuma kuyaishi maisha yetu kwa
 ukamilifu. Mtazamo huo ni kuyaona maisha kama zawadi, kila siku mpya 
unayoipata inakuwa kama nyongoza na hivyo unaitumia vizuri zaidi.
There are many who think that living is not painful, but superfluous. – Seneca.
Unapoiona
 siku mpya unayoianza kama nyongeza, unaitumia vizuri kwa sababu unajua 
huna uhakika kama utaiona siku nyingine kama hiyo. Huangalii jana 
ulifanya nini maana imeshapita, na wala huangalii kesho itakuwaje maana 
haipo, unachoangalia ni zawadi iliyo mbele yako.
Tukiweza
 kuziishi siku zetu kwa mtazamo huu, tutaacha kuona marudio 
yanayotuumiza na tutaanza kuona vitu vizuri vya kufanyia kazi. 
Mahali pengine Seneca amewahi kutuasa jinsi ya kuziishi siku zetu kwa ukamilifu, mfano ni nukuu hizi;
“Anza kuishi mara moja na ichukulie kila siku mpya kama maisha tofauti.”
“Nitaendelea kuyaangalia maisha yangu na muhimu zaidi nitaitathmini kila siku yangu kwa kufunga vitabu vya maisha kila siku.”
Kama
 kauli za Seneca zinavyosisitiza, usichukulie poa hii siku uliyonayo 
leo, kuna wengine wangetamani sana kuwa nayo lakini haijawezekana. Iishi
 kwa upekee wake, ipangilie vizuri na fanya mambo ambayo mwisho wa siku 
ukiyaangalia unajiambia kweli umeiishi siku hii.
Kila
 unapoimaliza siku yako, jifanyie tathmini, pitia kila ulichofanya tangu
 kuamka mpaka unaporudi kulala na kisha jiulize maswali haya matatu;
Moja; Ni yapi mazuri nimefanya leo na ambayo nitaendelea kuyafanya nikipata zawadi ya siku nyingine?
Mbili; Ni yapi mabaya nimefanya leo ambayo sitarudia tena kufanya kama nitazawadiwa siku nyingine?
Tatu; Yapi ambayo sijayafanya kwa ubora unaostahili na ambayo nitayaboresha zaidi nitakapopata zawadi ya siku nyingine?
Ukijiuliza
 maswali hayo matatu kila siku na kujipa majibu sahihi, kisha kuyafanyia
 kazi, maisha yako yatakuwa bora, hutazichoka siku zako, hutaahirisha 
chochote na utayazuia matatizo mengi kabla hayajawa makubwa.
Wenye hekima wanajua, maisha siyo mateso bali zawadi, ichukulie hivyo na utakuwa na maisha bora na tulivu.