Saturday, April 4, 2020

MFANYABIASHARA / MJASIRIAMALI : WSAIDIE WATEJA WALIOKWAMA

Huu ndiyo wakati mzuri kwako mfanyabiashara kuwaonesha wateja waaminifu kwako kwamba biashara yako inawajali, haiangalii tu kuingiza faida, bali inataka mteja aendelee kuwepo.
Kuna baadhi ya wateja wako watakuwa wamekwama kutokana na hali inavyoendelea, iwapo watakueleza kukwama kwao na ukawa na njia ya kuwasaidia, wafanya hivyo. Kwa sababu usipowasaidia na wao wakashindwa, basi biashara yako itakuwa imepoteza mteja moja kwa moja.

Mfano; kama kuna wateja umekuwa nao kwa muda mrefu na wamekuwa walipaji wazuri bila kusumbua, ila kipindi hiki wameshindwa kulipa kwa wakati, wape nafasi ya kuchelewa kulipa au kulipa kwa viwango tofauti na awali kama ipo ndani ya uwezo wako.

MFANYABIASHARA / MJASIRIAMALI : MIKAKATI YA UKUZAJI BIASHARA IENDELEE.

Wakati wa majanga kama haya, wengi huacha kufanyia kazi mikakati yao ya ukuzaji wa biashara. Kwa kuwa hali ya uchumi inakuwa siyo nzuri, wateja siyo wengi na waliopo hawanunui sana, wafanyabiashara huona hakuna haja ya kujisumbua, badala yake wanasubiri mpaka mambo yawe vizuri.
Kama tulivyoona mpaka sasa, hakuna mwenye uhakika mambo yatarudi sawa lini, inaweza kuwa kesho, wiki ijayo, mwezi ujao au mwaka ujao, hakuna ajuaye.
Hivyo wewe endelea na mikakati yako ya ukuzaji wa biashara kama vile hakuna mlipuko unaoendelea.
Endelea na mkakati wako wa masoko kwenye matangazo na hata kuwatembelea wateja kule walipo, mtaa kwa mtaa, ofisi kwa ofisi na nyumba kwa nyumba. Ila hakikisha unajikinga na kuikinga timu yako.
Endelea na mkakati wa mauzo kwa kuwashawishi wateja kununua na kununua zaidi ya walivyopanga kununua.
Endelea na mkakati wa utoaji wa huduma bora sana kwa wateja wako ili wanunue tena kwako na wawaambie watu wao wa karibu kununua
Mikakati hii inapaswa kufanyiwa kazi kila siku, iwe kuna majanga au hakuna. Hata kama huoni matokeo yake kwa haraka, usiache kufanya.

Mfano; mikakati ya masoko, mauzo na huduma kwa wateja kwenye kila biashara inapaswa kuendelea kama vile hakuna kilichobadilika, ila iendane na hali halisi ilivyo sasa.

MFANYABIASHARA / MJASIRIAMALI : JIHAKIKISHIE UPATIKANAJI WA MALI NA / AU MALIGHAFI.

Kama unafanya biashara ya kununua kwa jumla na kuuza kwa reja reja, unapaswa kujihakikishia upatikanaji wa mali katika kipindi hiki cha mlipuko. Kutokana na mipaka ya nchi nyingi kufungwa na shughuli kusimamishwa, hili linaathiri sana uzalishaji. Hivyo jipange mapema kwa kuhakikisha una mzigo wa kutosha katika kipindi cha mlipuko.
Kama unafanya biashara ya kuzalisha bidhaa, basi jihakikishie upatikanaji wa malighafi katika wakati huu wa mlipuko. Mabadiliko yanayoendelea yataathiri sana upatikanaji wa malighafi, jipange kwa kuhakikisha hilo haliathiri uzalishaji wako.

Mfano; wafanyabiashara wa bidhaa zinazotoka nje, kama nguo kutoka china, wamejikuta katika wakati mgumu kupata mzigo mpya tangu mlipuko huu uanze. Hivyo ni muhimu kuangalia njia nyingine ya kupata mzigo na kuhakikisha unapata mzigo wa kutosha kwa sababu hujui mlipuko huu utaisha lini.

MFANYABIASHARA / MJASIRIAMALI : TOA ELIMU NA USHAURI SAHIHI KWA WATEJA WAKO,

Kwenye mlipuko unaoendelea sasa, kila mtu ni mwalimu, mshauri na mtaalamu wa magonjwa ya mlipuko. Hata mtu ambaye mwezi mmoja uliopita alikuwa hajui (na huenda mpaka sasa) hajui kwamba kirusi siyo kiumbe hai kamili, ni mshauri mzuri sana kwa wengine kuhusu mlipuko unaoendelea.

Wewe wape wateja wako elimu sahihi, ambayo umeitoa kwenye vyanzo sahihi. Usilete ujuaji wako au kukusanya taarifa za mtandaoni na kufikiri hiyo ni elimu. Nenda kwenye vyanzo vya uhakika, na kwa hili la Corona, sikiliza taarifa za serikali na tembelea tovuti ya Shirika la Afya Duniani (WHO), kwa anuani www.who.int kupata elimu sahihi kuhusu mlipuko huu wa Corona.
Mfano; kuna vitu vingi ambavyo watu wanashauriana kufanya, ambavyo siyo sahihi. Kwenye tovuti ya WHO, kuna kipengele wanakiita MYTH BUSTERS ambapo wanatoa ukweli kuhusu vitu visivyo sahihi wanavyoshauriana watu. Kama ulaji wa vitunguu hauzuii maambukizi ya Corona. Ingia kwenye tovuti hiyo, pata taarifa sahihi na kisha washauri wateja wako kwa usahihi.

MFANYABIASHARA / MJASIRIAMALI : USITUMIE NAFASI HII KUNUFAIKA ZAIDI.

Katika hali ya mlipuko kama huu, ambapo watu hawana uhakika wa lini hali itarudi kama kawaida, wanakimbilia kufanya manunuzi makubwa. Hapa mfanyabiashara unapata tamaa ya kuongeza bei kwa sababu uhitaji ni mkubwa. Watu wanaweza kununua kwa bei juu kwa sababu hawana namna.
Lakini tambua kwamba huu mlipuko utapita, na kama unataka biashara yako iendelee kuwepo na iwe na wateja waaminifu hata baada ya mlipuko huu, usiutumie kujinufaisha zaidi.
Usiongeze bei kwa sababu tu kila mtu anaongeza bei na uhitaji ni mkubwa. Kama ulikuwa na mzigo wa kutosha kabla ya janga hili kuanza, endelea kuuza kwa bei zile zile. Na kama uhitaji ni mkubwa, wape kipaumbele wale wateja ambao umekuwa nao kwa muda mrefu.
Kama mlipuko umepelekea gharama za wewe kupata unachouza kuwa juu, waeleze wazi wateja wako kuhusu mabadiliko hayo. Usikimbilie tu kupandisha bei, jua wateja hawatasahau hilo na watavunja uaminifu kwenye biashara yako baada ya janga hili kupita.

Mfano; wauzaji wa vitu muhimu kama dawa, vifaa vya kujikinga, vyakula na vitu vingine wamekuwa wanapandisha bei katika nyakati kama hizi, wewe usifanye hivyo.

MFANAYABIASHARA / MJASIRIAMALI : JIKINGE WEWE NA TIMU YAKO.

Wewe mfanyabiashara ukiumwa au wasaidizi wako wakiumwa, biashara itaathirika zaidi. Hivyo wewe na timu yako mnapaswa kuwa mstari wa mbele katika kujikinga na maambukizi ya ugonjwa huu.
Hakikisha njia zote za kujikinga zinajulikana na kutumika na kila anayehusika kwenye biashara yako. Njia kuu zinafahamika, kunawa mikono kwa maji safi na sabuni, kuepuka kushikana, kuepuka kushika uso. Hivi vyote vinapaswa kufanyiwa kazi.
Pia eneo la biashara liboreshwe kwa namna ambayo linapunguza maambukizi. Ukaribu baina yako au watoa huduma na wateja unapaswa kupunguzwa. Maeneo ya kunawa mikono yanapaswa kuwepo au dawa za kusafisha mikono kupatikana kwa urahisi.
Usiache kujilinda wewe na timu yako kwa kuepuka gharama, ukiugua wewe au timu yako, ni tiketi ya kifo kwa biashara yako.

Mfano; kwenye kila eneo la biashara kunapaswa kuwa na sehemu ya watu kunawa mikono kwa maji na sabuni au kwa dawa maalumu. Pia kama biashara inahusisha watu wengi, kuwekwe utaratibu wa kupunguza msongamano wakati huu. Kwenye huduma za afya, watoa huduma wanapaswa kuwa na vifaa vya ziada vya kujilinda wao wenyewe.

MFANYABIASHARA / MJASIRIAMALI : BADILI MFUMO WA BIASHARA KUENDANA NA MABADILIKO YANAYOTOKEA.

Maisha ya watu yamebadilika katika wakati huu wa mlipuko wa ugonjwa wa Corona. Biashara yako pia inapaswa kubadilika ili kuweza kuwahudumia vizuri wateja wako.
Kama watu wanatumia muda mwingi nyumbani kuliko kutoka, usiendelee kusubiri wateja waje kwenye biashara yako, badala yake wafuate huko majumbani.
Badili mfumo wa biashara yako kutoka kusubiri wateja waje eneo la biashara na kufanya wateja waweze kuagiza wakiwa nyumbani na kupelekewa au kutumiwa kile walichoagiza.
Hatujui lini hali hii itaisha kwa hakika, hivyo usijiambie unasubiri mambo yatulie, badala yake chukua hatua sahihi ili uendelee kuwahudumia wateja wako.

Mfano; biashara ambazo zimekuwa zinategemea wateja waje kwenye biashara, ni wakati sahihi sasa kuweka mfumo wa wateja kuweza kuagiza wakiwa nyumbani na kisha kupelekewa au kutumiwa walichoagiza.