Monday, December 30, 2019

USIANZE SIKU YAKO KWA KUFUATILIA HABARI.

Habari nyingi ni hasi au zenye kuibua hisia kwa wafuatiliaji wake. Fungulia chombo chochote cha habari au tembelea mtandao wowote unaotoa habari na utaona habari gani zinapewa kipaumbele. Ni habari za kutisha au kusisimua. Habari za mauaji, ajali, mapigano, wizi, utekaji, ukatili na nyingine kama hizo.
Unapoianza siku yako kwa habari za aina hii, unavuruga kabisa akili yako. Unajikuta umepata hasira au kukata tamaa na kuona dunia haina maana. Hata mambo ambayo ulipanga kuyafanya hutaweza kuyafanya kwa hamasa kubwa pale ambapo umeshakutana na habari za kutisha au kukatisha tamaa.
Ndiyo maana nakushauri usianze siku yako kwa habari, sijakuambia usifuatilie kabisa habari (japo hilo ni jema ukiliweza), ila usianze nazo kwenye siku yako. Anza siku yako kwa kusali/kutahajudi, kusoma vitabu, kupangilia siku yako na kisha kuanza majukumu muhimu kwako kikazi au kibiashara. Mwisho wa siku wakati umeshakamilisha yale muhimu, hapo sasa unaweza kupitia habari ili ujue nini kinaendelea.
Ukifanya hivi utajikuta unakuwa na siku tulivu, siku ambayo umeweka umakini wako kwenye yale muhimu kwako kufanya na siyo kuvurugwa na habari za mambo yanayoendelea, ambayo hayakuhusu moja kwa moja.
Wapo wanaosema ni muhimu kuanza na habari kwa sababu kunaweza kuwa na kitu muhimu unapaswa kujua kabla siku haijaanza, labda kuna daraja limeharibika hivyo usipoanzana habari hutajua. Nasema hiyo siyo sababu yenye mashiko ya kuruhusu siku yako ichafuliwe na habari nyingi hasi. Na nikuambie kitu kimoja rafiki yangu, kama kuna habari muhimu kweli, itakufikia hata kama hufuatilii habari. Tukienda na mfano huo wa daraja kuharibika, hivi unafikiri unahitaji chombo cha habari kujua hilo? Kila mtu atakuwa anazungumzia hilo na hivyo utajua tu.
Kadhalika kwa habari nyingine ambazo ni muhimu, wale wanaokuzunguka watakuwa wanazizungumzia, hivyo kama ni kitu chenye umuhimu utakijua tu.
Usikubali kuharibu siku yako kwa kuanza na habari, anza siku yako kwa mipango yako na kisha imalize kwa habari.

PUNGUZA SANA AU ACHA KABISA KUTUMIA MITANDAO YA KIJAMII KAMA HAIKUINGIZII KIPATO

Mitandao ya kijamii imekuwa chanzo cha wengi kupoteza muda mwingi wa maisha yao. Pia imekuwa chanzo cha wengi kupata msongo na sonona kutokana na kufuatilia maisha ya wengine na kujilinganisha nao, kitu ambacho siyo sahihi kwa sababu wengi huigiza kwenye mitandao hiyo.
Hivyo ili kuepuka kupoteza MUDA  na  UTULIVU wako, na ili kupata AMANI ya moyo na kuepukana na msongo na sonona, acha kabisa kutumia mitandao ya kijamii. Jaribu hili , ile mitandao ambayo inachukua muda wako mwingi na kila ukiingia unatoka ukiwa unawaonea wengine wivu kwa mambo mazuri yanayoendelea kwenye maisha yao, acha kuitumia mara moja.
Ukiacha kutumia mitandao hii utajikuta ukiwa na muda mwingi wa kufanya kazi zako, kujifunza kupitia kusoma vitabu na hata muda wa kukaa na wale watu wa karibu na muhimu kwako.
Tumia mitandao hii ya kijamii kama tu inakuingizia KIPATO, kama unafanya biashara na unatangaza kupitia mitandao hii na inakuletea wateja, basi endelea kutumia kwa madhumuni ya biashara. Tofauti na hapo achana nayo.
Mitandao ya kijamii inaingiza fedha kupitia wewe, wewe ndiyo bidhaa inayouzwa na mitandao hii kwa wale wanaotangaza biashara zao. Hivyo kama na wewe huingizi fedha kupitia mitandao hii, achana nayo, usikubali kuuzwa kwa wengine.
Wapo wanaosema kama siyo mitandao ya kijamii hawawezi kukutana na maarifa mazuri kama haya. Hilo siyo kweli, maarifa mazuri yanapatikana pale unapoyatafuta, na mitandao ya kijamii siyo sehemu nzuri kwako kujifunza.
Hivyo acha kutumia mitandao ya kijamii 2020, labda kwa lengo la kibiashara pekee.

TOFAUTI KATI YA TAJIRI NA MASIKINI KATIKA KUJIFUNZA NA KUKUA...

MATAJIRI huwa wanajifunza kila siku na kuendelea kukua zaidi. Wanajisomea vitabu na kutafuta maarifa mbalimbali yanayowawezesha kupiga hatua. Wanaamini kuna mengi hawajui hivyo kujifunza zaidi, na hilo linawafanya wafanikiwe.
 
MASIKINI wao hawana muda wa kujifunza, wanaamini tayari wanajua kila kitu. Hawasomi vitabu ila habari za udaku na mitandao ya kijamii ndivyo wanapenda kufuatilia. Kwa njia hii wamekuwa hawajifunzi na hivyo kubaki kwenye umasikini wao.