Monday, May 27, 2019

UONGO TUNAOJIAMBIA KUHUSU MAFANIKIO NA KWA NINI HATUPENDI KUBADILIKA.

 Mwandishi anasema yapo mambo ambayo tumekuwa tunajidanganya sana kwenye mafanikio, na haya ndiyo yamekuwa yanachochea matatizo mengi tunayokutana nayo kwenye maisha. Baadhi ya mambo tunayojidanganya kwenye mafanikio ni haya; Tunajikadiria zaidi kwenye mchango wetu kwa mafanikio ya kile tunachofanya. Tunafikiri bila sisi mafanikio yasingepatikana, huku ni kujidanganya. Tunachukua sifa ambazo hatustahili kuchukua, kazi wamefanya wengine lakini wewe kama kiongozi ndiye unayetaka upewe sifa. Huwa tunajiona tuna ujuzi wa juu kuliko wale wanaotuzunguka. Huwa tunapuuza muda na gharama ambazo tumeshapoteza kwenye miradi ambayo haizalishi. Kukuza matarajio ya mafanikio ya mradi, kuwa na mategemeo makubwa kuliko uhalisia. Uongo huu ambao tumekuwa tunajiambia, hasa tunapokuwa viongozi kwenye kazi au biashara, unaathiri mahusiano yetu na wale walio chini yetu. Uongo huu unakuwa umetokana na mafanikio ambayo tunakuwa tumeyapata huko nyuma. Tunapopata mafanikio kidogo, huwa tunajiamini zaidi ya uhalisia. Kujiamini huku kulikopitiliza ndiyo kunawaingiza wengi kwenye matatizo na kuwazuia kufanikiwa zaidi.

Friday, May 24, 2019

FURSA 10 ZA KUTENGENEZA PESA FACEBOOK ------ " Fursa Afrika Mashariki Blog "

SHAUKU NI NGUVU ITAKAYOKUWEZESHA KUPATA CHOCHOTE KATIKA MAISHA YAKO.


Shauku ndiyo nguvu ya kwanza ya kukuwezesha kupata kile ambacho unataka kwenye maisha yako. Shauku ni ule msukumo wa ndani wa kukutaka upate kile unachotaka. Msukumo ambao hauondoki wala kupungua. Shauku ina nguvu kubwa ya kukusukuma kufanya mambo ambayo wengine wanaogopa, lakini kwako yanaonekana kawaida.

Watu wengi wamekuwa wanategemea hamasa iwafikishe kwenye mafanikio makubwa, lakini tatizo la hamasa ni huwa haidumu, mara kwa mara inabidi uchochee upya hamasa yako. Lakini shauku huwa haipungui wala kuhitaji kuchochewa, shauku unakuwa nayo muda wote na hii ndiyo inakusukuma wewe kupiga hatua zaidi.
 
Shauku inatokana na ile sababu kubwa inayokusukuma kupata unachotaka, ile KWA NINI inayokufanya wewe upambane kupata unachotaka. Kwa nini zinatofautiana kwa watu, wapo ambao wanafanya kwa sababu wamejitoa kuyafanya maisha ya wengine kuwa bora zaidi, wapo ambao wanafanya ili kuwaonesha wengine wanaweza na kadhalika.
 
Hakikisha una msukumo mkubwa ndani yako wa kukupeleka kwenye kile unachotaka, kwa sababu bila ya msukumo huu, hakuna nguvu nyingine itakayoweza kukusaidia kupata unachotaka.