Wednesday, June 25, 2025

JINSI YA KUCHAGUA WATU SAHIHI NA VITABU SAHIHI KWA MAENDELEO YAKO YA MIAKA MITANO IJAYO ?-----CALL / SMS / WHATSAPP + 255 716 924 136



 Baada ya kuelewa kuwa watu unaokutana nao na vitabu unavyosoma vina mchango mkubwa katika kukufanya mtu tofauti baada ya miaka mitano, swali linalofuata ni: unawachaguaje watu sahihi? Na unachaguaje vitabu vitakavyokujenga kweli?

Hii si kazi ya kubahatisha. Ni mchakato unaohitaji umakini, nidhamu, na maamuzi ya makusudi. Makala hii inakuonyesha njia ya kuchagua vyanzo hivi viwili vya mabadiliko ili kuimarisha safari yako ya mafanikio.


1. Jinsi ya Kutambua Watu Sahihi wa Kukua Nao

Kila mtu anayekuzunguka ana athari katika namna unavyofikiri na kutenda. Ili ukue:

a) Tafuta Watu Wenye Maono na Nidhamu

Watu wanaojitambua na wenye mwelekeo wa maisha hukupa msukumo wa kufanya makubwa. Hawapotezi muda kwenye manung’uniko au visingizio. tafuta watu wa namna hii rafiki yangu.

b) Watafute Waliofika Unakotamani Kufika

Kama kuna watu wamefikia mafanikio na hatu ambayo wewe unatamani kuwa umefikia, hawa ni washauri wa kweli. Wanaweza kuwa wafanyabiashara waliobobea, viongozi wa kiroho, au hata walimu wa kawaida lakini wenye hekima ya maisha. Ukiwapata watu wa namna hii kamwe usiwaachie, washikilie na uende nao ili wakusaidie kuweza kufikia ndoto zako kubwa.

c) Jihadhari na Watu Wanaopunguza Ndoto Zako

Wapo watu ambao kila mara huona sababu ya kwa nini jambo haliwezekani. wanadogosha lengo lako na ndoto zako. Wanaeneza hofu na mashaka. Epuka kuwaruhusu wawe sauti kuu katika maisha yako. Kumbuka kwamba ukikaa na waridi lazima utanukia. Sasa kazi ni kwako kuhakikisha kwamba unachagua waridi linalokufaa. La sivyo yeyote utakayechagua atakuwa sehemu ya maisha yako.

d) Jiunge na Mitandao ya Ukuaji

Kuna vikundi vya watu wanaojifunza pamoja – iwe ni vikundi vya kusoma, vya maadili ya kazi, au vya ujasiriamali. Huko ndiko mahali pa kukutana na watu sahihi.


2. Mambo ya Kuzingatia Katika Kuchagua Vitabu vya Kujenga Maisha Yako

Vitabu ni marafiki wasiochoka kukuinua. Lakini si kila kitabu kinajenga. Ili upate thamani:

a) Soma Vitabu Vinavyoendana na Malengo Yako

Kama lengo lako ni kuimarika kifedha, soma vitabu vya fedha. Kama unataka kuimarika kiroho, tafuta vitabu vya kiroho. Usisome tu kwa sababu “kila mtu anasoma.” Kumbuka vitabu vipo vingi na siyo vitabu vyote vinakufaa wewe. Kitabu ambacho kinasomwa na mwingine kinaweza kisiwe kizuri kwako, ndiyo maana wewe mwenyewe unapaswa kuwa mtu wa kuchagua kwenye hili suala.

b) Angalia Waandishi Wenye Matokeo Yanayoonekana

Soma vitabu vilivyoandikwa na watu walioishi kile wanachofundisha. Mfano: Mwandishi wa kitabu cha biashara ambaye ana biashara hai, au mshauri wa ndoa mwenye ndoa yenye afya.

c) Usipuuze Vitabu vya WASIFU NA TAWAFIFU (Biographies)

Kusoma maisha ya watu waliopitia magumu na kufanikiwa hukufundisha hekima ya kipekee isiyopatikana darasani. Wasifu wa watu kama Nelson Mandela, Wangari Maathai, Steve Jobs au Elon Musk unaweza kuwa chachu ya mafanikio yako. Hakikisha vitabu vya namna hii unakuwa navyo vingi na uvisome mara kwa mara.

d) Kuwa na Mpango wa Kusoma

Chagua angalau kitabu kimoja kwa mwezi, ukigawanya kwenye ratiba ya kila siku. Ni bora usome kurasa 10 kwa siku kwa nidhamu, kuliko kusoma kurasa 100 mara moja kisha ukaacha. Ukiweza kusoma kurasa kumi kila siku kwa mwezi utakuwa umeweza kusoma kurasa 300 kwa mwezi. Hii ndiyo kusema kwamba kila mwezi utakuwa unaweza kumaliza kitabu kimoja. Kwa mwaka utakuwa umeweza kumaliza vitabu siyo chini ya 12. Kwa hakika utakuwa unaweza kupiga hatua kubw aukilinganisha na asilimia kubwa ya watu ambao huwa hawasomi vitabu.


3. Chukua Hatua Leo: Unda Mazingira ya Mabadiliko

  • Fanya orodha ya watu watatu unaopaswa kuwasogelea kwa ajili ya kujifunza kutoka kwao.
  • Andika vitabu vitatu unavyotamani kusoma ndani ya miezi mitatu ijayo.
  • Anza sasa – usingoje “wakati mzuri.” Mabadiliko huanza pale mtu anapochukua hatua ya kwanza.

Watu sahihi ni daraja la mafanikio yako. Vitabu sahihi ni ramani ya safari yako. Usisubiri miaka mitano ikupite ukiwa bado palepale. Chagua kwa makusudi marafiki wa kukuinua na maarifa ya kukujenga.

Kwa hiyo, swali ni hili:
Leo unamruhusu nani akuathiri, na unasoma nini kila siku?

No comments:

Post a Comment